Header Ads

Mahakama Kuu Yaamuru Mwanafunzi wa UDOM Aliyefukuzwa Chuo kwa Kuongoza Mgomo Arudishwe Masomoni

MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dodoma imetengua uamuzi wa Baraza la Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) ya kumfukuza mwanachuo Phillip Mwakibinga na kuamuru arudishwe ili kumalizia masomo yake.

Uamuzi huo ulitolewa jana na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, John Chaba kwa niaba ya Jaji Awadhi Mohamed aliyekuwa akisikiliza shauri hilo.

Mwakibinga alikuwa akisoma Shahada ya Kiswahili mwaka wa tatu wakati akisimamishwa na alikuwa Waziri Mkuu wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii. Katika uamuzi huo, mahakama ilisema mlalamikaji hakupewa nafasi ya kusikilizwa na hivyo kukiuka haki ya asili ya mlalamikaji. Pia mlalamikaji hakupewa haki ya kusikilizwa na hakuandikiwa mashtaka rasmi.

“Baraza liliegemea upande moja bila kumhoji wala nafasi ya kusikilizwa na kujitetea,” alisema. 
Mwakibinga alifukuzwa Udom Januari 14, mwaka jana, kwa madai ya kuongoza mgomo ambapo siku hiyo baraza la chuo lilikaa na kumfukuza bila kupewa nafasi ya kusikilizwa.

Alifungua kesi Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma kutaka mahakama kutengua uamuzi huo. Kwa mujibu wa wakili wa Mwakibinga, Elias Machibya alisema awali waliomba ruhusa ya kufungua kesi na wakapewa Februari 5, mwaka jana wakiomba kutengua maombi ya baraza la Chuo Kikuu cha Dodoma.

“Tulipata kibali cha kufungua kuomba kutengua maamuzi ya Chuo Kikuu cha Dodoma kwa kumfukuza,” alisema.

Alizitaja sababu kuu tatu za kupinga mwanafunzi huyo kufukuzwa chuo kuwa ni pamoja na kutopewa nafasi ya kusikilizwa, hakuna hatua za nidhamu zilizochukuliwa, walimfukuza wakidai aliwahi kuhusika na migomo ya nyuma.
 Alidai barua ya kumfukuza ilisainiwa na Profesa Shaban Mlacha.

Januari 14, mwaka jana uongozi wa Udom ulimfukuza Mwakibinga ambaye wakati huo alikuwa Waziri Mkuu wa Serikali ya wanafunzi, Kitivo cha Sayansi ya Elimu ya Jamii, na kupewa barua ya kusimamishwa kutokana na kosa la kuhamasisha mgomo.

Uongozi huo ulisema Mwakibinga amefukuzwa kabisa kwa kuwa alishawahi kujihusisha na mgomo wa mwaka 2010/2011 akafukuzwa lakini akakata rufaa na kuomba msamaha kwenye Kamati nidhamu.

“Baada ya kukata rufaa Kamati ikamuonea huruma ikamrudisha kabla ya kurudi alitakiwa aje na kiapo kutoka kwa mwanasheria kwamba hatajihusisha na mgomo tena lakini akarudia tena kosa hilo."

Mwakibinga amesema amefurahia uamuzi huo kwani ndio sababu ya msingi ya kufungua kesi na mahakama imetenda haki. Alisema anasubiri barua ya hukumu ambayo itatoka kesho ndipo taratibu zake za kurudi chuo zitakapoanza.

No comments

Powered by Blogger.