Header Ads

Polisi Watinga Nyumbani kwa Gwajima....Mwenyewe Agoma Kufungua Mlango

Jeshi  la Polisi kwa mara nyingine jana lilizingira nyumba ya Askofu wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima, kwa kile lilichodai kuwa lilifika kufanya uangalizi.

Taarifa ambazo zimethibitishwa na Askofu Gwajima mwenyewe, zinaeleza kuwa polisi walifika nyumbani kwake wakiwa katika gari lao.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, polisi hao walipojaribu kutaka kuingia nyumbani kwa askofu huyo, walizuiwa mlangoni kwa sababu hawakuwa na kibali chochote wala maelezo yanayojitosheleza ya kutaka kukutana na kiongozi huyo wa kiroho.

Askofu Gwajima  jana alikiri polisi hao kumfuata nyumbani kwake na hivyo kulazimika kumtafuta wakili wake mara moja.

“Ni kweli walikuja wakiwa na gari la polisi, lakini walipofika nami nilimpigia mwanasheria wangu ambaye aliniambia tuwaulize wametumwa na nani na kama wana ‘search warrant’ (kibali cha kufanya upekuzi) au ‘arrest warrant’ (kibali cha kukamata),” alisema.

Askofu Gwajima alisema walipowauliza, walimtaja Afande Kingai kama ndiye mtu aliyewatuma, lakini hawakuwa na kibali chochote.

Kwa mujibu wa Askofu Gwajima, mwanasheria wake alifanya mawasiliano ya simu na Afande Kingai ambaye amepewa jukumu la kuwafuatilia wale wote waliotuhumiwa katika sakata la dawa za kulevya na kumuuliza sababu za kumfuata nyumbani.

“Afande Kingai amemweleza mwanasheria wangu kuwa walikuwa wamekuja kwa ajili ya ‘observation’ (uangalizi) tu, kwa hiyo mwanasheria wangu akasema kama ni ‘observation’ tu tusiwaruhusu kuingia ndani kwa sababu sheria ya hivyo hakuna, na sisi tumewazuia hawakuingia ndani,” alisema Askofu Gwajima.

Alipoulizwa kama kufuatwa kwake sasa na polisi kuna uhusiano wowote na kauli alizozitoa kanisani kwake hivi karibuni kuhusu elimu ya Paul Makonda ambaye ni Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Askofu Gwajima alisema huenda ikawa hivyo, lakini akasisitiza kuwa hana uhakika kwa sababu hajazungumza na askari waliomfuata.

Na alipoulizwa kama anadhani ujio huo pia unatokana na andiko ambalo linasambaa kwenye mitandao ya kijamii ambalo linasema Jumapili ijayo mwalimu aliyemfundisha mtu mmoja anayetajwa kwa jina la Bashite atakuwapo kanisani kutoa ushuhuda, Askofu Gwajima alikana akisema andiko hilo si lake.

Pamoja na hayo, Askofu Gwajima alikwenda mbali na kuhoji: “Hata kama ni kweli, sasa unaogopa mwalimu kuja… kanisani kwangu wapo watu wengi waliosoma naye Bashite kuanzia shule ya msingi na Sekondari ya Pamba… vyeti kama huna huna tu.”

Alipoulizwa haoni kauli yake kwamba Rais Magufuli ni tofauti kabisa na Makonda ilikuwa na nia ya kuwatenganisha viongozi hao, Askofu Gwajima alisema aliyemtaja kwa kumshambulia ni Makonda na si Rais.

“Aliyenitaja kwa kunishambulia katika sakata la dawa za kulevya ni Makonda na si Rais, mimi nimemuongelea Makonda, mimi ni mtumishi wa Mungu siwezi kuongozwa kwa ‘speculation’, si unajua hata Yesu alisema kama wewe huna dhambi basi uwe wa kwanza kushika jiwe,” alisema Askofu Gwajima.

Alipoelezwa kuwa katika mahubiri yake ni kama anaonekana kumshtaki Makonda, askofu huyo alisema: “Nilisema nitamshtaki kwa mahakama iliyo juu yake na nilisema Makonda aombe radhi, angekuwa mstaarabu baada ya sakata lile yeye mwenyewe angenipigia simu na kuniambia Gwajima nilikengeuka, lakini hajafanya hivyo.”
 
Pamoja na hayo, Askofu Gwajima alisema kwa aliyoyafanya Makonda tayari amekwishamsamehe na ndiyo maana hajampeleka mahakamani.

No comments

Powered by Blogger.